Please use this identifier to cite or link to this item: http://ir.mu.ac.ke:8080/jspui/handle/123456789/2402
Title: Utendaji wa kidrama wa riwaya ya haini ya Shafi Adam Shafi 2003
Authors: Munyioki, Anne Mwari
Keywords: Drama performance
Issue Date: Nov-2018
Publisher: Moi University
Abstract: Utafiti huu umeshughulikia utendaji wa kidrama katika riwaya ya Haini ya Shafi Adam Shafi (2003). Katika kuchunguza utendaji wa kidrama katika riwaya hii, tulibainisha vipengele vya utendaji vilivyotuwezesha kutathmini kuigizika kwa riwaya teule. Malengo ya utafiti huu ni pamoja na: Kubainisha lugha ya majibizano ilivyotumika na utendaji wa wahusika katika riwaya ya Haini, kuchanganua masimulizi ya kiutendaji na taswira za kifilamu katika riwaya ya Haini na hatimaye kutathmini ufaafu wa vipengele vya utendaji katika utendaji wa kidrama wa riwaya ya Haini. Kutokana na malengo haya, utafiti huu uliegemea nadharia tete kwamba lugha ya majibizano imetumika kwa kiwango kikubwa na wahusika watafanikisha utendaji wa kidrama wa riwaya ya Haini, kwamba masimulizi ya utendaji na taswira za kifilamu zimetumika katika riwaya hii na kwamba vipengele vya utendaji vitafanikisha utendaji wa kidrama wa riwaya teule. Utafiti huu umeongozwa na Nadharia ya Utendaji iliyoasisiwa na Wallace Bacon na kuendelezwa na Victor Turner na Richard Schechner. Nadharia hii inasisitiza kwamba pana uhusiano wa karibu kati ya utendaji na kazi ya kifasihi, na kwamba matini ya kidrama huwasilisha ujumbe wake vyema zaidi kupitia uigizaji wake kwenye jukwaa. Watafiti wa awali kuhusu suala la utendaji wameshughulikia utendaji katika fasihi simulizi, tamthilia na sanaa za maonyesho. Ingawa riwaya imetafitiwa kwa kina, tafiti nyingi ni zile zinazoegemea fani na maudhui. Tofauti na tafiti hizi, utafiti huu umejikita katika utendaji wa kidrama katika riwaya, mintarafu riwaya ya Haini ya Shafi Adam Shafi (2003). Huu ni utafiti wa kiuhakiki, na hivyo mbinu zilizotumiwa kukusanya data ni utafiti maktabani ambapo tulisoma riwaya teule kwa makini na kudondoa vipengele vya utendaji kama vinavyojitokeza. Pamoja na maktaba ya Margaret Thatcher ya Chuo kikuu cha Moi, tulizuru maktaba zingine, zikiwa pamoja na maktaba za Chuo Kikuu cha Nairobi na Kenyatta. Tulisoma makala mbalimbali zilizoandikwa kuhusu mada ya utafiti, vitabu na majarida. Hatimaye, tulitembelea mitandao na tovuti mbalimbali zinazozungumzia utendaji pamoja na kupakua makala mbalimbali yanayohusu utendaji. Mbinu ya kithamano ilitumika katika uchanganuzi wa data tuliyokusanya na kueleza matokeo ya utafiti. Matokeo ya utafiti wetu yalidhihirisha kwamba iwapo baadhi ya vipengele vya utendaji tulivyobainisha katika riwaya ya Haini vitafanyiwa ukarabati, utendaji wa kidrama wa riwaya hii utafanikiwa iwapo itafanyiwa ufaraguzi na kutendwa kwenye jukwaa. Mbali na utafiti huu kuweka wazi suala la mwingiliano tanzu (riwaya na drama), utaongeza maarifa yaliyopo kuhusu drama na fasihi kwa jumla.
URI: http://ir.mu.ac.ke:8080/xmlui/handle/123456789/2402
Appears in Collections:School of Arts and Social Sciences

Files in This Item:
File Description SizeFormat 
Munyioki Anne Mwari 2018.pdf927.17 kBAdobe PDFThumbnail
View/Open


Items in DSpace are protected by copyright, with all rights reserved, unless otherwise indicated.